Monday 10 June 2013

Nelson Madiba Mandela



Afrika Kusini. Shujaa wa mapambano dhidi ya utawala wa Kibaguzi, Rais mstaafu wa Afrika Kusini Nelson Madiba Mandela bado kalazwa  hospitalini kutokana na hali yake kuwa mbaya.
Madiba alilazwa tena baada ya hali yake kuwa mbaya kutokana na kupata tena maambukizi ya ugonjwa wa mapafu. Mandela mwenye umri wa miaka 94, ambaye mwaka 1994 alikuwa kiongozi wa kwanza mweusi kwa taifa hilo lenye nguvu kubwa kabisa za kiuchumi barani Afrika kutokana na uchaguzi wa kihistoria ulioshirikisha makabila yote, amewahi kulazwa hospitali mara tatu tokea mwezi wa Desemba

Taarifa ya Serikali ilisema kwamba amekuwa akikabiliwa na maambukizi hayo kwa siku kadhaa sasa.
juzi Serikali ilisema kwamba hali yake ilizidi kuwa mbaya saa moja na nusu asubuhi na ilibidi kupelekwa katika Hospitali ya Pretoria ambapo hali yake bado haijakuwa nzuri lakini iko thabiti.
Msemaji wa ofisi ya Rais Mac Maharaj alisema  madaktari waliwahakikishia kuwa  madiba yuko katika hali ya utulivu na kwamba ameanza kupumua mwenyewe.

Hata hivyo maneno yaliyotumiwa na Serikali hususan neno la hali yake kuwa “mbaya” ni sababu ya kuwatia wasiwasi wananchi milioni 53 wa Afrika Kusini ambao kwao Mandela anaendelea kubakia kuwa alama kuu ya mapambano dhidi ya miongo kadhaa ya utawala wa wazungu walio wachache nchini Afrika Kusini.
Mshindi huyo wa Tuzo ya Amani ya Nobel, alijiuzulu kuwa Rais  mwaka 1999 baada ya kuwepo madarakani kwa muhula mmoja na amejitenga na siasa kwa muongo mzima.
Mara ya mwisho alionekana hadharani wakati wa fainali za michuano ya soka Kombe la Dunia mjini Johannesburg hapo mwaka 2010.

No comments:

Post a Comment