Friday 14 June 2013

Bajeti yahiyooooooo... 2013/2014






 Bajeti yahiyooooooo!!!!!!2013
WAZIRI wa Fedha na Uchumi, Dk. William Mgimwa, amewasilisha bajeti ya serikali ya sh Trilioni 18.2 kwa mwaka wa fedha 2013/14 huku akiainisha vyanzo vipya vya mapato, kupunguza kodi na ushuru ili kuleta unafuu kwa wananchi.
Licha ya bajeti hiyo kutogusia kabisa suala la nyongeza ya mishahara ya watumishi wa umma, serikali imependekeza kupunguza kiwango cha kodi ya mapato ya ajira kutoka asilimia 14 hadi 13.
Akiwasilisha bajeti hiyo, iliyosomwa kwa saa 2.10, Mgimwa aliainisha vyanzo mbalimbali vitakavyoongeza mapato ya serikali lakini vingi vikiwa ni vilevile vya sigara, pombe, mafuta na magari wakati vyanzo vinavyohusu rasilimali za nchi kama madini, makampuni makubwa yakiendelea kuneemeka.
Waziri Mgimwa alisema kuwa ili kufikia malengo ya kiuchumi na mapato katika mwaka 2013/14 amependekeza kufanya maboresho ya sheria mbalimbali.
Sheria hizo ni pamoja na ile ya kodi ya ongezeko la thamani sura 148 akipendekeza kufuta msamaha wa VAT unaotolewa kwenye huduma za utalii, kutoa msamaha wa VAT kwa wazalishaji wa nguo nchini zinazozalishwa kwa pamba ya ndani kwa bidhaa na huduma.

“Kwa hatua hii mzalishaji wa nguo zinazotumia pamba ya hapa nchini hatalipa VAT kwenye manunuzi yake yote yanayohusiana na uzalishaji wa nguo hizo,” alisema.
Katika maboresho ya kodi ya mapato sura 332, Waziri Mgimwa alisema kuwa itaanzishwa kodi ya zuio ya asilimia 10 ya kamisheni ya usafirishaji wa fedha kwa njia ya simu za mikononi.
Pia watoa huduma mbalimbali kama vile za ushauri wa kitaalamu na nyinginezo watatozwa kodi asilimia tano bila kujali kama kuna namba ya utambulisho wa mlipa kodi (TIN) au la.
Aliongeza kuwa itatozwa kodi ya zuio kwenye bidhaa zinazonunuliwa na serikali na taasisi zake kwa kiwango cha asilimia 2 huku msamaha wa kodi ya zuio kwenye ukodishaji ndege kwa walipa kodi wasio wakazi ukifutwa.
Mgimwa alifafanua kuwa katika sheria ya ushuru wa bidhaa sura 147 maboresho yatalenga kuongeza kiwango cha ushuru wa biashara kwenye magari yasiyo ya uzalishaji ya umri wa zaidi ya miaka 10 kutoka asilimia 20 hadi 25.
Pia kuanzisha kiwango kipya cha ushuru wa bidhaa cha asilimia tano kwenye magari ya uzalishaji yenye umri wa zaidi ya miaka 10. Kwamba lengo la maboresho ya sheria hiyo ni kupunguza uingiza wa magari chakavu, kulinda mazingira na kupunguza ajali.
Waziri alisema ameongeza ushuru kwa mafuta ya dizeli kutoka sh 215 hadi 217 kwa lita huku ushuru wa petroli ukipanda kutoka sh 339 hadi sh 400 kwa lita na mafuta ya taa ushuru unabaki vilevile wa sh 400.30 kwa lita.
Baadhi ya wataalumu wa uchumi waliotoa maoni yao jana, walisema kuongeza ushuru kwenye bei ya mafuta ya petroli na deseli kutasababisha mfumko wa bei, hivyo kuzidisha maumivu kwa wananchi.
Katika kulinda viwanda vya ndani bidhaa za kutoka nje kama mazuria, vipodozi, mafuta ya kujipaka, bunduki na risasi, boti za kifahari, ndege na helikopta zitatozwa ushuru kati ya asilimia 2.5 hadi 10.
“Kutoza ushuru wa bidhaa wa asilimia 14.5 kwenye huduma zote za simu za kiganjani badala ya muda wa maongezi tu. Katika ushuru huu asilimia 2.5 zitatumika kugharamia elimu nchini,” alisema.
Katika mtiririko huo wa mapato, vinywaji baridi vimeongezeka kutoka sh 83 hadi 91 kwa lita, juisi ya matunda ya nchini kutoka sh 8 hadi 9, juisi ya matunda ya nje sh100 hadi 110, bia iliyotengenezwa kwa nafaka ya hapa nchini sh 300 hadi 341, bia zingine zote zimepanda kutoka ushuru wa sh 525 hadi 575 kwa lita.
Mvinyo wa zabibu za nchini utatozwa sh 160 kwa lita badala ya sh 145, mvinyo wa zabibu za nje ushuru umepanda kutoka sh 1,641 hadi 1,775 kwa lita, vinywaji vikali kutoka sh 2,392 hadi 2,631.
“Sigara zisizo na kichungi za nchini ushuru utapanda kutoka sh.8,210 hadi sh.9,031 kwa sigara elfu moja, sigara zenye kichungi za nchini zitapanda kutoka sh. 19,410 hadi 21,351 kwa siagara elfu moja,” alisema.
Kuhusu sheria ya usalama barabarani sura 168, marekebisho yatagusa kuongeza viwango vya ada ya mwaka ya leseni za magari ambapo gari lenye ujazo wa ijini 501.cc-1500.cc itapanda kutoka 100,000 hadi 150,000.
Mgimwa aliongeza kuwa gari lenye injini 1501.cc-2500.cc itapanda kutoka sh. 150,000 hadi 200,00 wakati gari la injini zaidi ya 2501.cc itapanda kutoka 200,000 hadi 250,000 huku injini chini ya 501cc ambayo ni ya bodaboda na pikipiki haitatozwa kodi.
.

No comments:

Post a Comment