Wednesday 14 August 2013

WANAOTAFUTA KAZI NI WENGI, AJIRA NI CHACHE

 WANAOTAFUTA KAZI NI WENGI,
 AJIRA NI CHACHE


Wakala wa Huduma za Ajira Tanzania (TAESA), imesema inakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwamo kutokuwa na fursa za kazi za kutosha ukilinganisha na idadi ya wahitimu/watafuta kazi waliopo katika soko la ajira.

Akizungumza mwishoni mwa wiki, jijini Dar es Salaam, Msemaji wa TAESA, Peter Ugater, alisema kwa sasa wahitimu na watafuta ajira wamekuwa ni wengi kulinganisha na nafasi za kazi zilizopo. Alizitaja changamoto nyingine kuwa ni kutokuwa na rasilimali za kutosha kuwezesha kufikia malengo ya wakala, watafuta kazi wengi kuwa na matarajio makubwa kuliko hali halisi ya soko la ajira, pia baadhi ya waajiri na watafuta kazi kutotumia huduma za wakala nchini.

Katika kukabiliana na changamoto hizo, Peter Ugater alisema TAESA ina mikakati mbalimbali kama vile kukusanya, kuchambua na kusambaza taarifa za soko la ajira na kuendeleza rasilimali watu ili kuongeza tija na ufanisi.

Nyingine ni kuendelea kuwaunganisha watafutakazi na waajiri ndani na nje ya nchi na kufanya utafiti katika Nyanja za upatikanaji wa fursa za ajira pamoja na kuendelea kuainisha wakala binafsi kwa lengo la kutoa huduma hiyo nchi nzima.

Pia, Ugater alisema mpaka sasa TAESA imeshawahudumia jumla ya wateja 13,188 kati yao ikiwa watafutakazi 1,229, waajiri 830 na wakala binafsi 60 na kuendesha vipindi kwa watafutakazi 426 kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kuhimili ushindani na changamoto zilizopo katika soko la ajira.

No comments:

Post a Comment